inspire

inspire

Lebo

AFYA (8) AJIRA (5) BIASHARA (39) ELIMU (14) MAHUSIANO (2) MALEZI (16) MAZINGIRA (12) SAIKOLOJIA (48) VIJANA (7)

Business registration

Green Consulting

business consultancy

business consultancy

Business consulting-2

Business consulting-2

Professional Consulting

PDC

Swahili translator

Swahili translator

TANGAZO-KITABU

E-BOOK: MTAZAMO WAKO NI UPI?

TANGAZO:Kitabu kipya. Kitabu! Kitabu!Kinauzwa Katika Maduka Ya Vitabu.Pia M-Pesa 0754 572 143, Tigo Pesa 0716 075 826.Ili Kikufikie Ulipo, Tafadhali Ongezea Sh.10,000/- .... TANGAZO:Kitabu kipya. Kitabu! Kitabu!Kinauzwa Katika Maduka Ya Vitabu.Pia M-Pesa 0754 572 143, Tigo Pesa 0716 075 826.Ili Kikufikie Ulipo, Tafadhali Ongezea Sh.10,000/- ....

TANGAZO TUWEZESHANE

TANGAZO TUWEZESHANE

DARDY'S INVST-20/10/2017

DUNIA IKUONE

DUNIA IKUONE

Jumamosi, 30 Mei 2015

MAZINGIRA: KUELEKEA SIKU YA MAZINGIRA DUNIANI JUNI 5


Kama ilivyo ada kila mwaka, tarehe 5 Juni duniani kote tunaungana kwa sauti moja na kauli mbiu moja kuadhimisha siku hii muhimu kwa mustakabali wa maisha yetu; kwa kuzingatia kuhifadhi na kuitunza “nyumba” (mazingira) inayotutunza.
Siku hii muhimu duniani ilianzishwa katika Mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN General Assembly) mwaka 1972.Hivi leo “Siku Ya Mazingira Duniani” inaendelea kuheshimiwa duniani pote pia kusimamiwa kikamilifu na Kitengo cha Umoja wa Mataifa cha Mazingira-United Nations Environment Program (UNEP).Tukiwa kama familia moja duniani, husindikizwa na kauli mbiu itolewayo kila mwaka kwa kuzingatia maoni ya wataalam na wadau wa Mazingira duniani.
Kwa bahati nzuri kauli mbiu ya mwaka huu isemayo“Seven Billion Dreams.One Planet.Consume With Care kwa tafsiri ya lugha ya Kiswahili-Ndoto bilioni saba. Sayari moja.Tumia kwa uangalifu inatukumbusha kutumia rasilimali tulizonazo kwa uangalifu ukizingatia kuwa kuna ongezeko la idadi ya watu duniani (bilioni 7 hadi sasa) wenye ndoto tofauti tofauti, mabadiliko ya tabia nchi na wakati huo huo rasilimali nyingi zilizopo si rejereshi; zinatumika na hazijirudii au kurudishwa tena.
Shirika hilo la Umoja wa mataifa linalohusika na Mazingira duniani (UNEP) limeweka angalizo kuu kuwa kutokana na mfumo wa maisha ya binadamu, na uhitaji wa rasilimali ambazo kwa kiasi fulani zinaelekea kutokidhi ongezeko la idadi ya watu duniani; kuna hatari kubwa kuwa kama hali itaendelea kama kawaida kwa kuangalia makisio ya ongezeko hilo la watu bilioni 9.6 ifikapo mwaka 2050 tutahitaji kuwa na sayari 3 ili kukidhi mahitaji yetu.Unashangaa! Ndiyo huko tunakoelekea na vizazi vyetu. Wengine naona wameanza kuangalia uwezekano wa kuishi kule kwenye sayari ya “Mars”.Mimi na wewe je? Natania tu…
Imefika wakati wa kuamka sasa, kila mtu kuchukua wajibu sasa, kufanya pale anapoweza kuhakikisha kuwa rasilimali zilizopo zinatumika kwa uangalifu mkubwa kwa kuzingatia maendeleo endelevu- maendeleo yanayokumbuka na kuchukua taadhali kubwa kuwa kuna vizazi vijavyo vitakavyohitaji rasilimali zilizopo sasa.Ni maendeleo yanayozingatia manufaa ya jamii, mazingira yenyewe na uchumi kwa ujumla wake.Maendeleo yanayosahau kimoja kati ya hivyo vitatu, si maendeleo endelevu; yanapaswa kukosolewa, kubezwa na kuzomewa kwa kelele nyingi.Anza sasa!
Imetayarishwa na
Mwandishi wa Kitabu-“Mtazamo Wako Ni Upi?”
Imetolewa na
Jielimishe Kwanza!

Alhamisi, 21 Mei 2015

AJIRA: UHURU WA KUUNDA NA KUJIUNGA NA VYAMA VYA WAFANYAKAZI

-->
Picha na www.eventbrite.ca

UTANGULIZI.
Uhuru wa kujumuika unawapa wafanyakazi uhuru wa kuunda na kujiunga na vyama vya wafanyakazi. Vilevile unawapa wafanyakazi haki ya kushiriki katika shughuli za vyama vyao kwa uhuru bila hofu ya kubaguliwa au kunyanyaswa au kupoteza haki yoyote.
Hata hivyo, uhuru wa kuunda na kujiunga na vyama vya wafanyakazi una mipaka yake. Uhuru huu umewekewa mipaka kwa wafanyakazi wa kada zifuatazo:-
a)    Mahakimu – hawa wanaweza kuunda na kujiunga na Chama cha Maafisa wa Mahakama pekee.
b)   Waendesha Mashitaka – hawa wanaweza kuunda na kujiunga na chama cha Waendesha Mashitaka au Watendaji wengine wa Mahakama pekee.
c)    Wafanyakazi wa kada ya Meneja Mwandamizi ambaye kwa nafasi yake ana mamlaka ya kutengeneza sera kwa niaba ya muajiri na ana mamlaka ya kuingia majadiliano na Chama cha Wafanyakazi, haruhusiwi kujiunga na Chama cha Wafanyakazi wasio Mameneja Wandamizi.
Pia uhuru wa kuunda na kujiunga na vyama vya wafanyakazi unatoa kinga ya mfanyakazi kutobaguliwa na mtu yeyote kwa sababu ya kuwa mwanachama wa chama cha wafanyakazi au kujihusisha na shughuli halali za chama.
HAKI ZA CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
1.   Kuwa na Katiba yake bila kuingiliwa na dola, chama cha siasa au muajiri.
2.   Kupanga na kuendesha mambo yake ya ndani na shughuli halali bila kuingiliwa.
3.   Kujiunga na kuunda shirikisho na kushiriki shughuli za shirikisho hilo.
4.   Kujiunga na mashirikisho ya kimataifa, kuchangia na kupokea misaada ya kifedha kutoka kwa vyama au mashirikisho hayo. 
UTARATIBU WA KUUNDA CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
Kwa mujibu wa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini na.6 ya mwaka 2004, Chama cha Wafanyakazi kinaweza kuanzishwa na wafanyakazi wasiopungua 20. Wafanyakazi hao wanapaswa kuitisha kikao cha kuanzisha Chama, ambapo watajiorodhesha na kutia saini zao katika rejista ya mahudhurio. Watamteua Katibu wa kikao ambaye atatayarisha muhtasari wa kikao wenye azimio la kuanzisha chama.
MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA KUANZISHA CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
1.   Chama kiwe ni chama halisi cha Wafanyakazi (Bona fide Trade Union).
2.   Kisiwe chama kwa madhumuni ya kupata au kutengeneza faida (Association not for Gain).
3.   Kiwe ni chama huru, kwa maana kwamba kisianzishwe na muajiri au waajiri au serikali.
4.   Kianzishwe na wafanyakazi wasiopungua 20.
5.   Kiwe na katiba na kanuni zinazozingatia kifungu cha 47 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini na.6 ya 2004.
6.   Kiwe na jina lisilofanana na jina la chama kingine, kuzuia mkanganyiko au kuwapotosha watu.
7.   Kiwe na makao yake makuu ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
UTARATIBU WA KUSAJILI CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
Chama cha Wafanyakazi kinapaswa kusajiliwa ndani ya miezi sita (6) kuanzia tarehe ya kuanzishwa kwake. Maombi ya usajili yatafanyika kwa kujaza fomu maalum ambayo itajazwa kikamilifu na kusainiwa na katibu wa kikao kilichoanzisha chama hicho.
Fomu hiyo ya maombi inapaswa kuambatana na nakala zilizothibitishwa za rejista ya mahudhurio, na nakala zilizothibitishwa za katiba na kanuni, na kuziwasilisha kwa msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na waajiri.
MAJUKUMU YA CHAMA KILICHOSAJILIWA.
Chama kilichosajiliwa kinapaswa kuwasilisha kwa msajili kila ifikapo tarehe 31 Machi au kila mwaka taarifa zifuatazo:-
a)    Taarifa ya fedha zilizokaguliwa kwa kipindi cha fedha kinachoishia tarehe 31 Desemba ya mwaka uliopita.
b)   Orodha ya wanachama inayoonesha jumla ya wanachama kwa kipindi kinachoishia tarehe 31 Desemba ya mwaka uliopita.
c)    Majina ya viongozi walioteuliwa au kuchaguliwa na anuani zao ndani ya siku 30 tangu uteuzi au uchaguzi kufanyika.
d)   Mabadiliko ya kanuni ndani ya siku 30 kuanzia siku ya mabadiliko hayo.
Chama pia kina jukumu la kutunza kwa miaka isiyopungua mitano kumbukumbu zifuatazo:-
1.   Orodha ya wanachama katika fomu maalumu.
2.   Mihtasari ya Vikao.
3.   Karatasi za kura.

Chama cha Wafanyakazi kinapaswa wakati wote kutekeleza shughuli zake kwa mujibu wa katiba, kanuni na mazoea. Endapo itatokea chama kimeshindwa kuzingatia katiba yake, msajili au wanachama wanaweza kupeleka maombi mahakama ya kazi kutengua suala hilo lililofanyika kinyume na katiba.
Kabla ya maombi hayo kupelekwa mahakamani, taratibu za ndani ya chama ni lazima zifuatwe kwanza. Isipokuwa ikiwa ni kwa maslahi ya chama, basi maombi hayo yanaweza kupelekwa mahakamani bila kufuata utaratibu wa ndani wa chama.
HAKI ZA CHAMA CHA WAFANYAKAZI MAHALI PA KAZI.
Chama cha Wafanyakazi kilichosajiliwa kina haki zifuatazo mahali pa kazi:-
1.   Haki ya kuingia eneo la muajiri – kwa lengo la kusajili wanachama, kuwasiliana na wanachama, kufanya vikao na wanachama, kuendesha uchaguzi. (Kifungu cha 60 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini na.6 ya mwaka 2004).
2.   Makato ya Ada – kupokea ada za wanachama baada ya muajiri kuwakata kutoka kwenye mishahara yao. (Kifungu cha 61 cha Sheria ya Ajira).
3.   Kuwa na wawakilishi wake mahali pa kazi – chama cha wafanyakazi kinayo haki ya kuwa na wawakilishi mahali pa kazi kwa kuzingatia idadi ya Wanachama kama ifuatavyo:-
a)    Wanachama wasiozidi tisa (9) – muwakilishi mmoja.
b)   Wanachama kuanzia kumi (10) mpaka ishirini (20) – wawakilishi watatu.
c)    Wanachama kuanzia ishirini na moja (21) mpaka mia moja (100) – wawakilishi kumi.
d)   Wanachama zaidi ya mia moja (100) – wawakilishi kumi na tano, miongoni mwao watano lazima wawe wanawake kama wapo na ni wanachama.
MAJUKUMU YA WAWAKILISHI WA CHAMA MAHALI PA KAZI.
1.   Kuwawakilisha wanachama kwenye vikao vya kushughulikia malalamiko na nidhamu.
2.   Kuwasilisha hoja kwa niaba ya wanachama kuhusiana na kanuni, afya, usalama na ustawi wao.
3.   Kushauriana na muajiri kuhusu tija mahali pa kazi.
4.   Kukiwakilisha chama wakati wa ukaguzi na uchunguzi unaofanywa na wakaguzi kwa mujibu wa sheria yoyote ya kazi.
5.   Kuhakikisha kazi za chama kwa mujibu wa katiba ya chama.
6.   Kuendeleza uhusiano mzuri kazini.
7.   Kutekeleza majukumu waliokubaliana na muajiri.
Wawakilishi wa chama wanayohaki ya kupewa muda wa kutosha kutekeleza majukumu yao bila kukatwa mshahara na wanayo haki pia ya kupewa na muajiri taarifa zote muhimu zitakazowawezesha kutekeleza majukumu yao kikamilifu. Haki hizi zitatolewa na kutekelezwa vizuri bila kuvuruga kazi.
LIKIZO KWA WAWAKILISHI WA CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
Wawakilishi wa chama mahali pa kazi wanayo haki ya kupewa likizo ya malipo na muajiri kwa ajili ya kuhudhuria mafunzo yanayohusiana na majukumu yao. Hali kadhalika viongozi wa chama cha wafanyakazi na wa shirikisho ambalo chama ni mwanachama, wanayo haki ya kupata likizo ya malipo kwa ajili ya kutekeleza majukumu yao ya chama au shirikisho.
UTARATIBU WA KUPATA HAKI ZA CHAMA.
Chama cha Wafanyakazi kilichosajiliwa kutekeleza haki za chama, kinapaswa kumtaarifu muajiri kwa kujaza fomu CMA F3 kikianisha haki ambazo kinataka kuzitekeleza pamoja na mahali pa kazi ambapo kinataka kuzitekeleza haki hizo.
Muajiri akishapokea fomu hizo anapaswa kukutana na chama ndani ya siku 30 ili kufikia makubalianao ya pamoja yatakayotoa haki hizo, na kuweka utaratibu wa kuzitekeleza. Endapo hakutakuwepo makubaliano au muajiri atashindwa kukutana na chama ndani ya muda uliowekwa, chama kinaweza kupeleka mogogoro huo mbele ya Tume kwa ajili ya usuluhishi.
Usuluhishi ukishindikana chama kinaweza kupeleka mgogoro huo Mahakama ya Kazi kwa uamuzi.
USITISHAJI WA HAKI ZA CHAMA CHA WAFANYAKAZI.
Haki za chama zinaweza kusitishwa iwapo chama kitakiuka makubaliano ya msingi ya utoaji haki hizo au kwa amri ya mahakama inayotoa haki hizo.
Ikitokea hali hiyo ya ukiukwaji wa makubaliano, muajiri anaweza kupeleka mgogoro huo mbele ya Tume kwa ajili ya usuluhishi. Usuluhishi ukishindikana, muajiri anaweza kupeleka mgogoro huo Mahakama ya Kazi akiiomba Mahakama isitishe makubaliano ya kutoa haki hizo au iondoe amri yake ya kutoa haki hizo
HITIMISHO.
Mara nyingi katika maeneo ya kazi kumekuwa na migogoro mingi sana inayohusu masuala ya haki za vyama vya wafanyakazi. Waajiri kwa kutokujua au kwa makusudi wamekuwa wakikataa kutoa haki za chama kwa wafanyakazi wanachama wa vyama vya wafanyakazi. Hali hii imekuwa ikipelekea kuibuka kwa migogoro hiyo ambayo huatarisha mahusiano mazuri kati ya muajiri na wafanyakazi.
Mara nyingine wanachama wamekuwa wakizitumia haki zao vibaya katika maeneo yao ya kazi, jambo ambalo pia linamfanya muajiri kutoridhika na hali hiyo ambapo pia hupelekea migogoro ya kikazi kuibuka.
Makala hii imelenga kutoa ufafanuzi na uelewa juu ya mambo mbalimbali yanayohusu Vyama vya Wafanyakazi na Haki zilizomo kwa pande zote mbili (muajiri na wafanyakazi). Aidha imeainisha majukumu ya chama na wanachama kwa ujumla.
Ni matumaini yangu kuwa itasaidia kutoa uelewa kwa wadau wa sekta ya ajira, hasa waajiri na wafanyakazi na hivyo kusaidia kupunguza migogoro ya kikazi na kuimarisha mahusiano mazuri kati ya wadau hao.
Imeandaliwa na Emmanuel C. Zongwe kwa msaada wa vitabu mbalimbali, mitandao na uelewa binafsi katika masuala ya Ajira na Mahusiano Mahala pa Kazi.

Simu: +255 (0) 717 058 045/ +255 (0) 755 223 697

E-mail: ezongwe@yahoo.com

Imetolewa na 
Jielimishe Kwanza.





Jumapili, 10 Mei 2015

MTAZAMO: HIVI NDIVYO WANAVYOFANYA WENGINE KUKUAMINISHA WANACHOAMINI KWA MASLAHI ZAO BINAFSI…Kuwa Makini Kutambua Viashiria Vifuatavyo.

Makala inayofanana: NJIA TANO (5) ZA KUWAFANYA WATU WENGINE WAKUAMINI  KWA NIA NJEMA KABISA.


Ndugu msomaji na mfuatiliaji wa Jielimishe Kwanza Blog, unapaswa kujua kuwa kuna watu au makundi ya watu hapa duniani hutumia njia za ujanja ujanja na pia kuchanganya na saikolojia ya maisha ya binadamu ili kujinufaisha.Hutumia ujanja huo kuwaaminisha wengine wanachoamini na mwisho wa siku hutumia migongo na ufikiri hafifu wa wengine kujineemesha.
Bila kificho nakuletea viashiria VITANO (5) ili kukuweka wazi ndugu msomaji na ujue kuwa katika viashiria hivyo vinavyoainishwa unataka kutumika au unatumika kwa maslahi ya wengine.

1.SIKU ZOTE HUONYESHA KUWA NA MAMLAKA
Katika kila mahojiano na majadiliano yenu huonyesha kuwa ni wenyewe pekee wanaoweza kutatua tatizo husika kwa wakati husika. Hivyo kukufanya uwe mtu wa kusindikiza mawazo na matakwa yao.
2.WANAAMINI SANA MAWAZO YAO NA KUBEZA YA WENGINE…
Kiashiria hiki hakina tofauti sana na namba 1, tofauti ni kuwa wao hupenda kupuuza na kubeza mawazo ya wengine wazi wazi kwa makusudi na baadaye huyatumia yale ya msingi kwao kwa manufaa binafsi.
Ni watu walio mafundi wa kukatisha tamaa kwa kutumia maneno yenye uzito katika hali iliyo halisi.Hutumia takwimu kwa namba halisi na nukuu mbali mbali kubeza mawazo ya wengine.
3.WANAJIAMINI SANA KWA YALE WANAYOYASEMA BILA KUBADILIKA BADILIKA
Kujiamini ni silaha yao kubwa.Wanaelewa maana halisi ya kujiamini kwa kile wanachoeleza na ni rahisi kwao kukuaminisha wanachoamini kwa matakwa binafsi.
4.HUJENGA HOJA NZITO KUPITIA HOJA YAKO
Huunganisha kiashiria hiki na kiashiria namba 2; kubeza mawazo yako lakini kwa upande mwingine hutumia hoja yako kutoa hoja nzito iliyo na maslahi kwao.
5.HUONYESHA MAPUNGUFU YA KATIKA HOJA ZAKO
Ni mahili sana wa kuchunguza na kuelezea mapungufu ya wengine katika lugha ambayo utaridhika.Mwisho wa siku hutumia mapungufu yako na kuyaboresha kwa manufaa yao binafsi bila hata kukushirikisha.
_________
Ndugu msomaji wa makala hii usifikiri watu hao ni “magenius” au wana uwezo wa kipekee kwa kupendelewa na Mungu; La hasha! Ni wepesi tu wa kujifunza, kujielimisha kwanza na kusoma vitabu mbali mbali vilivyosheheni maafunzo na uzoefu wa maisha ya watu waliofanikiwa kwa kupitia saikolojia ya maisha ya binadamu.
Kazi kwako, je unataka kuendelea kutumika na hao wajanja kwa maslahi zao binafsi au unachukua hatua ya ujasiri kubadilika na kuhama hapo ulipo kifikra na kimtazamo? Jibu unalo!
Makala hii imeandaliwa kwa kutumia ubunifu na uelewa binafsi wa kisaikolojia wa mwandishi Henry Kazula  kwa kushirikiana na vitabu mbali mbali vya kisaikolojia.

Imetolewa na
Jielimishe Kwanza

Jumapili, 3 Mei 2015

MTAZAMO: NJIA TANO (5) ZA KUWAFANYA WATU WENGINE WAKUAMINI KWA NIA NJEMA KABISA.

-->
Picha imetolewa na www.eppgroup.eu
Mafanikio yako katika kuwagusa wengine kwa mawazo yako ni ule uwezo binafsi wa kuwafanya wengine wakuamini.Pia jinsi ya kuwasiliana na kufuatilia mazungumzo na wengine hujenga uwezo na hali ya kuaminika kwa wengine.
Hata siku moja huwezi kutimiza azma yako ya kufikisha mawazo yako kwa wengine kuhusu biadhaa, huduma au suala lenye mustakabali kwa maendeleo ya jamii kama tu hawakuamini au huaminiki.
Ni sawa kabisa kuwa watu wanaweza kukusikiliza kwa makini lakini wasitendee kazi mawazo au ushauri wako; hii ndiyo hali halisi hadi watakapopiga hatua nyingine ya ujasiri kukuamini kwa kuwaaminisha kupitia vile ulivyo sanjali na unayoyasema.
Ukiwa muuzaji bidhaa, je watu watanuua bidhaa yako kama hawaiamini? La hasha! Inatakiwa uweze kuwaaminisha umuhimu na ubora wa bidhaa. Katika kuweka msisitizo wa jambo hili, Mwandishi wa kitabu “Start With Why”-Simon Sinek anasisitiza kwa kusema kuwa;  “People don't buy what you do; they buy why you do it. And what you do simply proves what you believe”. Katika tafsiri ya Kiswahili-“Watu hawanunui unachofanya, hununua kwa nini unafanya unachofanya.Unachofanya hutosha kuwaaminisha unachoamini”.
Ukiwa kama mkuu wa ofisi (Manager), unayetaka wengine wakubaliane na matakwa yako au utaratibu fulani; utaanza kujiuliza, je wananiamini? Hii ni kwasababu kama hujajenga hali ya kuaminiwa, ama kwa hakika hakuna atakayetekeleza matakwa yako.
Kwa upande mwingine kama mzazi, je watoto wako wanaamini unapowaambia, usifanye hiki mwanangu? Je, watoto wetu wanajutia unapowaeleza kuwa umewaeleza mara nyingi kuhusu kutofanya jambo fulani lakini wanakaidi?
Ijulikane kuwa, kazi ya kuwaaminisha wengine si rahisi kama huna ujuzi au mbinu stahiki.Kuwaaminisha wengine si jambo la mazoea au mzaha mzaha. Lakini kwa bahati nzuri leo napenda kutoa zawadi hii kwako msomaji kuwa kuna njia TANO (5) rahisi sana unazoweza kuzifuata kama nilivyozinukuu kutoka katika kitabu cha “Secrets of Power Persuasion” cha Roger Dawson ili kuijenga na kuinua hali yako ya kuaminika kwa wengine na kujiongezea heshima, uthamani na utendaji katika maisha yako ya kila siku. Zifuatazo ni njia TANO (5) katika dondoo, zitakusaidia sana kama utazitumia;
DONDOO 1:
“Never assume they believe you”.
USIBASHIRI KUWA UNAAMINIWA
Watu wenye nguvu ya kuwahamasisha na kuwaaminisha wengine kwa mawazo yao wana mambo matatu (3) kuhusu kutobashiri;
1)   Kutobashiri hali ya umasikini wao: kutobashiri kuwa hawawezi kulipia gharama ya bidhaa inayouzwa
2)   Kutobashiri kuwa umeeleweka
3)   Kutobashiri kuwa umeaminika. Hili jambo la mwisho ni la msingi sana. “Kutobashiri kuwa umeaminika”.
Hakikisha unagusia masuala yote ya msingi kwa kuzingatia kuwa watu unaotaka wakuamini nao wanakusikiliza kwa makini na kutafakari kwa kina kuhusu unayowaeleza na kukuamini.Tumia kila mbinu kuhakikisha unaeleweka ili wengine wakuamini. Ni lazima uonyeshe uwezo wa kutekeleza kile unachotaka wengine waamini na kutekeleza.
Dondoo hii inasisitiza; narudia tena na tena-Usibashiri kuwa umeeleweka au kuaminiwa na wengine.
DONDOO 2:
“Only tell them as much as they’ll believe”.
WAELEZE KADIRI UWEZAVYO HADI WAKUAMINI
Dondoo hii inamaanisha kuwa usiwaeleze watu zaidi ya vile unavyofikiri ili wakuamini.Kiuhalisia kabisa unaweza kuwa na bidhaa au huduma inayozidi mategemeo au matarajio ya wateja, lakini kama utashindwa kuwafanya wakuamini, hutakuwa na wakumlaumu.
DONDOO 3:
“Tell the truth, even if it hurts”.
WAELEZE UKWELI MTUPU HATA KAMA UNAUMA
Ni kweli kabisa kueleza au kuelezwa ukweli inauma.Kama ulikuwa hufahamu maana halisi ya kueleza ukweli ni vyema ukaanza sasa utawafanya wengi wakuamini.Haijalishi ni ukweli mchungu kiasi gani, usisite! eleza kila kitu wazi wazi.Hakika narudia tena, utaaminiwa kibiashara, kiutendaji na kimaisha kwa ujumla.
DONDOO 4:
 “Point out the disadvantages”
ONYESHA MAPUNGUFU YA WENGINE KIUTENDAJI
Ukiwa ni mtu wa kutoa au kuonyesha mapungufu ya bidhaa au huduma za wengine au utendaji wa mtu fulani ni dhahiri kuwa lolote utakalosema baada ya hapo litaaminika au kuaminiwa na wengine.Tafiti zimeonyesha kuwa kuna faida NNE (4) nzito kwa kukosoa au kutoa mapungufu ya upande mwingine kimtazamo;
1)                  Huufanya upande unaokosolewa kuamini kuwa huna unafiki,ubaguzi wala upendeleo.Pia ni mtu wa haki uliye na upeo mpana katika kushauri wengine kutenda na kuenenda katika unyoofu.
2)                  Humfanya msikilizaji ajione kuwa unamthamini na kuamini uwezo wake kiakili hivyo kuweza kuyaona mapungufu yake na pia kujiona ni mkosaji kupitia ukosoaji wako.
3)                  Hukuhamasisha na kukulazimisha kutarajia mambo halisi yasiyo na mapungufu hivyo kujitahidi kufanya mahojiano yenye kujenga
4)                 Inakuongezea sifa ya kukubalika na kuaminika katika kila utalosema.
DONDOO 5:
“Use Precise Numbers”
ONGEA UKITUMIA TAKWIMU KWA NAMBA HALISI
Watu huamini zaidi  takwimu kwa namba halisi na si makisio au makadirio kwa namba.Takwimu unazotoa kwa namba halisi zitakuongezea hali ya kuaminika zaidi kwa wale wanaokusikiliza.Hii huonyesha ni jinsi gani unavyoeleza mambo kwa uhakika na ufasaha. Hivyo basi, ukitaka kujijengea hali ya kuaminika, tumia namba halisi.Mfano, unaweza kusema kuwa kampuni yako inaweza kuongeza mapato yake kwa asilimia 75 kuliko kusema kampuni inatarajia kuongeza mapato yake  kwa takribani mara mbili ya yale ya mwaka jana.
Nakutakia utekelezaji mwema katika kujijengea uwezo wa kuaminika na kila mtu.
Makala hii imeandaliwa kwa kutumia ubunifu na uelewa binafsi wa kisaikolojia wa mwandishi Henry Kazula kwa kushirikiana na uzoefu kutoka katika kitabu cha “Secrets of Power Persuasion” cha Roger Dawson.
Imetolewa na
Jielimishe Kwanza.